Header Ads

KWA NINI TUNAVAA…?


Mwalimu wangu wa shule ya msingi alinifundisha ya kuwa mahitaji muhimu ya mwanadamu katika maisha yake ni chakula, malazi na mavazi. Huenda wahenga hawa walotajirika busara, hekima na adili za kupindukia waliona ni kwa namna gani mavazi yana umuhimu mkubwa katika maisha ya mwanadamu.

Bila haka mwanagenzi wa kisiwa cha kiswahili utakubalina nami ya kuwa mavazi yaani nguo ni ishara tosha kabisa ya busara, hekima na maadili.  Hii ni sababu yangu binafsi, lakini nilijaribu pia kuzungumza na wadau mbalimbali juu ya suala la uvaaji.

Nilipomuuliza kijana Abdillah yeye alinijibu kwa mujibu wa Quran Tukufu akasema. Katika Quran tukufu mathalani surat AL A’raaf (aya ya 26), Allah anasema “Enyi wanaadamu tumekuteremshieni nguo (mavazi) kwa ajili ya kuficha tupu zenu (kuhifadhi miili yenu na sehemu za siri) na pia tumekuteremshieni nguo kwa jili ya mapambo, na vazi la uchamungu ambalo ndio bora kuliko mavazi yote. Hapa sikutia neno zaidi.

Lakini pia nilipata wasaa na kuzungumza na kijana John Yunde, pia alinijibu kwa mujibu wa biblia kutoka katika kumbukumbu la Torati ( 22: 5) mwanamke asivae mavazi yampasavyo mwanaume, wala mwanaume asivae mavazi ya mwanamke, kwa maana kila afanyaye mambo hayo  ni machukizo kwa bwana wake.

Baada ya kupata nukuu hizo kutoka kwa vijana hao wema, nilijitafakari kwa muda kisha nikawaza na kuwazua je kwa nini tunavaa? Sasa mwanagenzi fuatana nami ili tujue kwa nini tunavaa?
Kumbe dhumuni la kuvaa ni kujisitiri, kusitiri siri zetu, siri zilizobeba aibu na maana kubwa ya uwepo wetu hapa katika mgongo wa ardhi. Lakini pia nimejifunza ya kuwa kuna taratibu za uvaaji kumbe watu wa jinsi ya kiume basi wavae kianaume na wale wenye jinsi ya kike wavae kike kama Mola wetu Mlezi alivyoagiza.

Najaribu kutafakari jinsi kizazi cha sanaa, kizazi cha nyoka, kizazi cha dotcom kinavyovaa sasa hivi, yaani hakuna uvaaji wenye kufuata taratibu wala kanuni yoyote ile yaani tunavaa tu, vile tunavyojisikia. Suala hili lilinipa msukumo na nguvu kuweza kuzungumza na vijana wenyewe ambao mpira huu wanatupiwa wenyewe. Nilifanya mjadala mfupi na vijana Rweymam David, Jackline Christopher, Flora Primo, Hawa Makweba na Omar Mpondi.

Niling;amua kwa vijana hawa wao wanadai kuwa ni hulka ya kijana mwenyewe, ulimbukeni huku wengine wakidai kuwa ni athari za utandawazi. Lakini kwa upande mwingine wa shilingi walikemea vikali uvaaji huu wa kihuni. Ukistaajabu ya Mussa utayaona ya Firauni, kumbe hata mavazi yana mahala pake, yaani kuwa katika kumbi za starehe ama ufukweni wao wamebariki kuwa yafaa mtu kuvaa kisasa kuvaa hovyo lakini ukiwa sehemu rasmi basi ni sharti uvae kiheshima, sasa swali ninalobaki nalo ni Je, mwili wa mwanadamu kuna maeneo unatakiwa kuhifadhiwa wakati sehemu nyingine uadhirishwe?
Suala la uvaaji wa mlegezo yaani kuteremsha suruali mahala ambapo si pake huo ni uhuni usiovumilika, tena haupaswi kuvumiliwa hata kwa nukta moja ya muda. Hili ni suala baya sana kwani tunakiuka maagizo ya Mwenyezi Mungu juu ya suala la kujisitiri kusitiri mwili.
 Lakini je vipi kuhusu hawa mabinti wanaovaa sketi ama gauni fupi, huu pia ni ugonjwa  ambao unapaswa kupingwa na kila nafsi inayoishi katika sayari hii ya tatu.

Tunapokiuka kanuni za uvaaji tujue kabisa ni kujishushia heshima, ni utovu wa nidhamu na ni maandilizi ya kujenga kizazi kilichopotea, hivyo nitoe shime kwa kila kiumbe mwenye kuitwa binadamu na mwenye akili timamu aweze kulipinga suala hili.

Turejee katika maadili ya uvaaji mzuri, pia suala la kubadilishana mavazi, huyu wa kiume avae ya kike na wa kike avae ya kiume hii si sawa hata kidogo. Suala la kwenda na wakati si uvaaji mbovu, si kubadili taratibu za mavazi. Ni kujisitiri mwili. Tusisingizie joto au mazingira tukumbuke lengo la kuvaa ni nini? kama tutapuuzia haya basi hatutakuwa tofauti na wanyama ambao hawana habari na mavazi.


Hakuna marefu yasiyo na ncha, basi nami nisiseme sana, haya kwa leo yanatosha. Waswahili tunasema mwenye macho haambiwi tazama na mwenye masikio haambiwi sikia. Bila shaka tumesikia lakini mja ni kunena muungwana ni vitendo hivyo tuchukue haya tuyabebe vifuani mwetu tuyafanyie kazi ili tuweze kurejea lengo la kuvaa.

No comments

Powered by Blogger.