Header Ads

TAARIFA YA MGANGA MKUUU MOROGORO KUHUSU AJALI YA TRENI NA COASTER ILIYOTOKEA LEO ASUBUHI


IKIWA imepita takribani miezi mitatu tangu wanafunzi wa Shule ya Lucky Vincent ya Mkoani Arusha wapate ajali na watu 35 kupoteza maisha, leo majira ya saa moja asubuhi, treni ya abiria iliyokuwa ikitokea Bara imegongwa na basi la abiria aina ya Coaster lenye namba za usajili T 438 ABR katika eneo la TANESCO, mjini Morogoro.

Coaster hiyo inayofanya safari zake kati ya Morogoro mjini na Kihonda ilikuwa imebeba wanafunzi wa shule tofauti wakielekea shuleni, mmoja wao anadaiwa kupoteza maisha huku wengi wao wakijeruhiwa kutokana na ajali hiyo tofauti na taarifa zilizosambaa mwanzo kuwa watu watatu walikuwa wamefariki.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini humo, Mganga Mkuu wa Hospital ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro, Dkt. Frank Jacob amesema leo asubuhi amepokea maiti ya mwanafunzi mmoja na majeruhi kadhaa ambapo wawili kati yao hali zao ni mbaya.

Baada ya kutokea kwa ajali hiyo mwandishi wetu alifika haraka eneo la tukio na kukuta umati mkubwa wakimshushia kichapo dereva wa daladala hiyo ambaye jina lake halikupatikana mara moja wakati akitaka kukimbia baada ya tukio hilo.

Umati wa wananchi wa Morogoro umejazana nje ya hospital hiyo kwa lengo la kuwashuhudia majeruhi hao, pia uongozi wa Mkoa wa Morogoro upo hospitalini hapo.

No comments

Powered by Blogger.