Header Ads

MWANAMKE MWENYE SURA TANO.


Mwanamke ndiyo nguzo ya familia, nguzo ya jamii, nguzo ya taifa na ni nguzo ya dunia. Ninapotamka matamshi haya ninakuwa na uhakika na kupata nguvu za kutembea kifua mbele kwani ninajua kabisa hakuna eneo nililobanmanga maneno.

Sifa za mwanamke zipo lukiki sana, kila sifa nzuri anayo mwanamke na kila mwanamke anapaswa kujichukulia kama mwanamke na hana haja ya kupambana kuwa sawa na mwanamke. Kwa sasa naweza kusema ya kuwa manuari iliyobeba kizazi cha wanawake inaennda mrama. Hii ni kwa sababu leo wanawake wengi katika sayari pekee hii iliyotunukiwa viumbe hai ndani mwake wanapambana kuwa wanaume. Inachekesha lakini inasikitisha pia.

Tena zimetokea taasisi, asasi na mashirika mbalimbali kutoka katika kila kona ya ulimwengu zikidai zinapambana kuhakikisha wanawake kuwa sawa na wanaume. Mmmh wacha nicheke kwa kuwa nina kila sababu ya kufanya hivyo, wanawake hawawezi kuwa sawa na wanaume hilo jambo halipo tena halipo. Halipo kwa sababu mwanamke ni mwanamke na mwanaume ni mwanaume. Mungu ameumba hivyo nasi tupo hivyo.

Badala ya kuendeleza mijadala, midahalo, semina ama warsha za kumjengea ghorofa la mawazo na fikra potofu kuwa mwanamke awe sawa na mwanaume. Kitu ambacho aghalabu ni lulu kwa sasa ni kuhakikisha kuwa mwanamke anavaa vazi la heshima, vazi takatifu, vazi ambalo Mola Mlezi amemtabaruku. Na si vazi jingine bali ni vazi la uanamke. Hilo ndilo haswa linamfaa linamtosha na linampendeza zaidi ya hilo analolitaka sasa.
Ama kuhusu kichwa cha Makala hii ni sura tano za mwanamke, hakika mwanamke anazo sura tano kwa mtazamo wangu lakini ikiwa ni sura nne tu zenye kumpendeza na hiyo moja ni ya bandia ambayo inamfanya atoke katika taswira ya mwanamke na kubaki katika kibonzo tu cha mwanmke.

Sura ya kwanza ni Mwanamke dada. Kila mwanamke anayezaliwa lazima apitie katika surah ii. Ni sura ambayo huvaliwa punde tu baada ya fikra za mwanadamu huyu kuwa amepevuka kiakili na kukua kimwili na kuweza kupembua mbichi na mbivu. Ndiyo haswa buwa kama bawabu itakayompa mtu ruhusa ya kuingia katika hatua nyingine za makuzi. Katika surah ii mwanamke anapaswa kujifunza kuwa nadhifu kwa matendo, mawazpo na mavazi kiasi kwamba kuwa kiigizo kwa wadogo zake, lakini kuwa Johari kwa wazazi wake, pia kuwa lulu kwa jamii hatimaye kuwa tunu ya taifa huku akitwaa taji la umalkia wa ulimwengu.

Sura ya pili ni mwanamke mke. Ndiyo hapa namzungumzia mwanamke mke. Hakuna mwanadamu ambaye ni mkamilifu lakini katika surah ii mwanamke anapaswa kuwa muadilifu wa kupindukia, hapa anapaswa kuwa na hazina ya kutosha ya hekima. Huku akimiliki bustani kubwa ya uvumilivu lakini hayo yote tisa, kumi anapaswa kuvaa medali ya upendo moyoni. Kulingana na uzito wa surah ii, mwanamke hapa anavaa majukumu mazito ya kumlea mumewe, kuwalea wanawe, kulea ndugu lakini hapa anakuwa ni bawabu inayoumnganishwa nguzo za mlango na mlango wenyewe. Lugha tamu yenye ukarimu iliyochanganyikana na upole ndiyo humfanya mke kuwa mke bora yaani mke mwema. Kama mwanamke akiivaa surah ii barabara basi dunia nzima itakuwa sawa na kijito kidogo kilichojificha na mharamia huku samaki wakazi wakiwa katika furaha ya maisha.

Sura ya tatu ni mwanamke mama. Hapana shaka kila mtu katika bongo zake anaijua hii sura. Kwa kuwa baada a mtu kuolewa basi kifautacho ni mtu kuwa mama. Hivyo mwanamke mke akitunukiwa ujauzito, akapewa kinga kisha akafanikiwa kutoa kiumbe aitwaye binadamu salama kutoka katika tumbo lake na kumleta katika mgongo wa dunia basi huwa mama. Uchungu wa mwana aujuae mama, kama hivi ndivyo mamabo yalivyo basi sina shaka kuwa mwanamke akiwa mama lazima ajue majukumu yake. Jukumu lenye uzito ni hili la malezi.Ukisikia mwanamke anamwita mwanwe mbwa wewe, bila shaka mwanawe atakuwa mbwa ndogo na huyo mama ndiye mbwa mkubwa. Basi mwanamke anapaswa kutambua ya kuwa kuwa mama siyo jambo la kubebwa na kidole kidogo cha mkono. Unapokuwa mama tunajua utahakikisha kuwa familia imekula imeshiba tena imekula vinono, pa iwe safi kwa mwili na tabia lakini wewe ndiyo kiungo wa familia. Pia wewe ni mwalimu wa kwanza wa familia, wewe ndiye mlezi na wewe ndiyo njia ya kukifikisha kizazi chako kwenye mikono salama. Basi usihakikishe wanao wanakuwa na tabia mbovu maadili duni na utu dhaifu.

Sura ya nne ni mwanamke kiongozi. Baada ya kuwa mama wa familia yaani kiongozi wa familia bila shaka hatua ifuatayo ni kuwa kiongozi na si mtawala. Jane Radier ni mwanamke shupavu, jasiri mwenye kiremba cha uongozi lakini name nimvishe joho la umalkia kwani yeye hutambua kwa kaisi kikubwa nafasi ya mwanamke kama kiongozi na bila shaka ni moja kati ya kina Mama Samia wa baadaye. Kujiheshimu kimavazi na kuwa na adabu ya mazungumzo, kuishi kwa malengo, kuwa mwajibikaji, kujali muda hayo ni tisa na kumi ni kuwa na hofu ya Mungu ndiyi kutamfanya mwanamke kuwa kiongozi bora. Sambamba na hayo mwanamke lazima awe na uthubutu, kukubali kukoselewa nako ni sehemu ya nguzo zinazojenga nyumba imara ya mwanamke kiongozi. Kwa kuwa alizungumza Jane mimi nisiwe mwenye kutia chumvi zaidi kwani nikizidi kusherehesha nitakuwa mwathilika wa ile methali ya Kiswahili isemayo mapishi mengi huharibu radha ya chakula au miruzi mingi humpoteza mbwa hapo naweka nukta.

Sura ya mwisho ni mwanamke bandia. Kwa nini uwe bandia? Kwa nini usiwe halisia? Huu ni mtihani (mrundikano wa maswali) ambayo majibu yake kila mtu anayo kwenye hifadhi ya bongo yake kichwani. Mwanamke hapaswi kuvaa kama mwanamume, hapaswi kuwa na roho ya korosho (roho ya kwa nini). Kuishi kwa kuiga siko kuzuri kwani mwishowe kutakuja kukushinda na kuibukia kuwa kituko hatimaye kubaki kusema majito ni mjukuu. Mwanamke napaswa kuwa kama kito cha dhahabu ghali king’aacho kila wakati na kinachovutia nyoyo na mato ya watu wengi. Ukiishi vile unavyopaswa kuishi basi huna haja ya kung’anini kuketi kiti kimoja na mwanaume. Acha mwanaume awe mwanaume na wewe uwe ulivyo.



Kutokana na sura hizo tano za mwanamke bila shaka sasa kutakuwa na maswali machache. Lakini mwenye kuelewa tayari atakuwa ameelewa ni wapi pa kuchagua, ni wapi pa kupuuza na ni wapi pa kukimbilia. Mwanamke hapswi kukombolewa na shirika, asasi, taasisi wala mdau yoyote bali anapaswa kujikomboa mwenyewe na kama atafauata misingi na kanuni za maisha ya kike basi hutosikia katu suala la ukombozi wa mwanamke. Wacha nafsi zijililie zenyewe ndiyo kauli inayofunga nayo kwa leo huku nikikitaka binti wa kitanzania kuwa na vazi lako la kike linakutosha, linakupendeza na dnilo litakalokultea heshima mbele za watu.

No comments

Powered by Blogger.