"MAMAYANGU ALIUZA POMBE ILI APATE ADA YANGU YA SHULE"-SIMBU
Kuna usemi usemao ‘mafanikio hayaji kirahisi, lazima
uyapambanie’. Usemi huu unakamilishwa na mtanzania aliyeshinda medali ya
shaba kwenye mashindano ya IAAF World Championship 2017 Alphonce Felix
Simbu ambaye alimaliza katika nafasi ya tatu.
Simbu licha ya kuzaliwa na kulelewa katika familia yenye maisha
magumu hakuacha kupambana kwa kile anachokiamini na hatimaye amefanikiwa
kupata medali kwenye mashindano ya riadha ya dunia.
Mkimbiaji huyu amesimulia kwa ufupi maisha aliyopitia katika familia
yake licha ya vikwazo na magumu kadhaa lakini hakukata tamaa kwa kile
alichokiamini.
“Wakati nasoma nilipokuwa nikirudi nyumbani kwa ajili ya likizo,
nilikuwa nachelewa kurudi shule kwa sababu ya kukosa ada. Mama alikuwa
anauza pombe ili apate pesa ya kulipa ada.”
“Baba alikuwa akisaidiana na mama kuchota maji kwa ajili ya kuandaa pombe, walikuwa wanasaidiana kuhangaika kwa ajili yangu.”
“Huwezi amini, nilikuwa naiombea pombe ili iwe nzuri mama auze apate pesa ili mimi niwahi shule.”
Mwaka 2016 Simbu alihojiwa kwenye mashindano ya
Olympic Rio 2016 nchini Brazil akasema, lengo lake ni kuwa bingwa wa
Dunia wakati huo alimaliza katika nafasi ya tano.
Watanzania wote wanafurahia medali ya Simbu, hakika amelipambania taifa na kurudi na heshima kubwa. Hongera Alphonce Simbu.
No comments