Header Ads

DARASA LA NJE YA DARASA


Darasa ni darasa, darasa ni ukurasa, sina budi kuunasa, kama darasa la anasa hilo ndilo darsa linalotutesa lakini kitu cha kutambua ni kwamba darasa la nje ya darasa ni muhimu kuliko darasa la  ndani ya darasa. Je darasa la ndani ya darasa ni nini hasa?

Basi mwanagenzi wa Kisiwa cha Kiswahili hili leo naomba tutete kidogo juu ya umuhimu wa darasa. Tumezoea kusikia ya kuwa wazee wetu hasa wale tunaowaita wahenga ni wajuvi sana wa busara tena wana utajiri mkubwa wa maadili, ndipo hapo tunapata wasaa wa kusema ya kuwa ya kale ni dhahabu, na palipo na wazee haliharibiki jambo.

Siki hizi utamaduni wa Bwana Koloni yaani huyu mzungu aliyetufundisha ushenzi akatuletea ujinga na sasa ametuangamiza katika janga kubwa janga linatutafuna sisi na vizazi vyetu. Sisemi kuwa hakuna matunda matamu yenye virutubisho tuliyovuna kutoka kwake la hasha! Yapo tena yapo mengi sana.

Natafakari hapa kwa kuona jinsi alivyotuletea elimu ya kukaa darasani, huenda sina weledi wa kuweza kugundua siri iliyomo ndani ya maudhui ya elimu yake lakini kila nikiona wale wanaojinasibu kuwa wameelimika ndio hao hasa huonekana kama waliopotoka katika jamii yetu ya nchi ya rutuba wa uoto wa kijani.

Tazama jinsi wanafunzi wa usasa wanaojinasibu kuwa wamepata elimu yao darasani tena lile darasa la koloni, jinsi wanavyovaa, jinsi wanavyootembea, jinsi wanavyozungumza na jinsi wanavyoigiza maisha badala ya kuishi maisha halisi. Leo hii wamekuwa ni watu wa ajabu, watu wa kumtupa Mungu si wale wa kumpokea Mungu. Swali langu ni kuwa elimu yao imewafunza nini? Leo maisha ya kijirani yapo hatarani, maisha ya kusaidiana yapo kwenye kaa la moto hata salamu sasa imekuwa kama shilingi inayochezewa karibu na tundu la choo.

Najiuliza sasa hivi ulimwengu umehamia kiganjani. Hivi ni Kiganjani? Aah ndiyo kwani ndipo hasa skanu zinapoishi, kuna rafiki yangu aliwahi kuniuliza habari za skanu nikamwambia ndiyo hizo wanaita Smartphone. Ndizo hasa zimefikia hatua ya kuifanya dunia hii ikaitwa kijiji ha ha ha yaani leo ulimwengu wa Mungu umekuwa sawa Kijijini kwetu Ibambo kama haileti maana basi italeta laana.

Sasa hii elimu inayofunza watu watu zinaa, inafunza watu wizi tena wizi wa mali za umma, kuibia wasakatonge kina Chiku na Kapili waliolelewa kimasikini, elimu inayomfanya mtu amsahau baba mbaya zaidi wanamsahau hadi mama aliyewabeba tumboni kwa miezi tisa, haya ni majonzi makubwa.

Labda niseme tu tatizo siyo elimu lakini ni elimu ya darasani yaani ndani ya darasa, lakini je, vipi kuhusu elimu ya nje ya darasa?
Waswahili tuna misemo bwana mathalani huu wa usiache mbachao kwa msala ulipatao. Yaani leo sayansi na teknolojia ya Bwana Koloni ndiyo imegeuka msala, msala wenye kupita. Vipi kuhusu zile adili za Mtemi Mirambo, vipi kuhusu zile nasaha za Chifu Mkwawa. Tazama leo zimekuwa mbachao na watu wanaziacha.

Ninachokifahamu mimi kuhusu elimu ya nje ya darasa. Elimu inayotufunza kuvaa vema, elimu inayotufunza kusalimu kila mtu, elimu inayotunabaishia maisha ya kijirani. Ubinanadamnu ni huruma bwana. Utu ni upendo. Utaifa ni uzalendo, lakini yako wapi haya leo?
Kizazi kimekuwa hayawani yaani kilichokosa haya, leo mzee wa kaya ndiye hasa anatukuza umalaya. Kizazi kimekuwa kizazi kilichopotea. Kimetumbukia kwenye korongo kimezama mtoni ona hata hakielei baharani.

Sasa wanagenzi mwenzangu waswahili husema kusema sana si kumaliza, lakini ubora wa mzuingumzaji ni yule mwenye kuzungumza kwa uchache wenye busara. Basi nami nikhitimkishe kwa kusema kuwa ni muhimu kupata elimu ya nje ya darasa ile elimu unayotolewa na mjomba, shangazi, jirani baba na pengine hata mama elimu Ya nje ya darasa.
……………………………………………………………………………………………………

No comments

Powered by Blogger.