SIMBA HAIWEZI KUSHINDA BILA YA OKWI: TAMBWE
MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Yanga,
Mrundi, Amissi Tambwe, amefurahishwa
na matokeo ya bila kufungana ambayo
Simba iliyapata juzi Jumamosi ilipocheza
na Azam FC.
Hata hivyo, Tambwe ambaye msimu wa 2013/14
alikuwa akiitumikia Simba, alisema kuwa
alijua kabisa timu hiyo isingepata matokeo
mazuri katika mechi hiyo bila ya uwepo wa
Mganda, Emmanuel Okwi kwenye mchezo huo.
Akizungumza nasi Tambwe alisema kuwa
kwa washambuliaji wa Simba waliopo hivi
sasa, ukimwondoa Okwi, ilikuwa ni ngumu
kwao kuifunga Azam kutokana na kutokuwa
na ubunifu wa kutafuta ushindi pindi wanapokuwa
wamebanwa vilivyo na mabeki wa timu pinzani.
“Matokeo hayo nimeyapokea vizuri na nimefurahi
baada ya kuona kile nilichokuwa nikiwaza
akilini kwangu kimetimia, kwani nilijua kabisa
Simba wangekutana na matokeo hayo katika mchezo huo.
“Hiyo ni kwa sababu washambuliaji wengi wa timu
hiyo siyo wabunifu wa kutafuta mbinu mbadala za
kufunga pindi wanapokuwa wamebanwa vilivyo na wapinzani wao.
“Mchezaji pekee ambaye angeibeba Simba katika
mechi hiyo alikuwa ni Okwi lakini baada ya kusikia
tu kuwa hatacheza mechi hiyo moja kwa moja
matokeo hayo waliyopata yakanijia akilini kwangu,
” alisema Tambwe na kuongeza:
“Kwa hivyo hivi sasa dalili ya sisi kuchukua
ubingwa wa ligi kuu kwa mara ya nne mfululizo
nimeanza kuiona na ninamwomba Mungu nirejee
mapema uwanjani ili niweze kuisaidia timu yangu
ya Yanga kutimiza ndoto yetu hiyo.”
No comments