MGODI WA MWADUI WAFUNGWA
Uongozi wa Kampuni
ya Williamson Diamonds Limited
(WDL) umesitisha kwa muda
baadhi ya shughuli za uzalishaji
katika mgodi huo.
Taarifa ya uongozi wa mgodi
huo kwa wafanyakazi
jana, zilisema huduma
za uzalishaji zimesimamishwa
isipokuwa huduma maalumu
za ulinzi, tiba, umeme, maji,
zimamoto na usafiri unaohitajika
katika huduma hizo.
Taarifa hiyo ilisema huduma za
utawala zitaendelea
kufanya kazi wakati huduma
nyingine zitakazoendelea
kuendeshwa na mgodi
itatolewa taarifa uzalishaji
utakaporejea.
Taarifa hiyo ilisema Kampuni
ya WDL inasubiri agizo la
kuacha kusafirisha nje
almasi yake kutoka mgodini,
kifurushi namba W1-FY18.
Hata hivyo, taarifa za ndani
zinasema Serikali imezuia
kusafirisha kifurushi hicho
kwa misingi ambayo haijawasilishwa
rasmi kwao licha ya kuona taarifa
hizo kupitia vyombo vya habari.
“Hatuwezi kutoa maoni yoyote
kutokana na matokeo ya uchunguzi huo.
“Vifurushi vyote vinavyosafirishwa
kwa biashara nje hukadiriwa thamani
yake hapa mgodini na watumishi
wa ‘TANSORT’ ambacho ni kitengo
cha kukadiria thamani ya almasi
na vito wanaowawakilisha
Wizara ya Nishati na Madini.
“Kifurushi kinavyosafirishwa
kinapigwa mihuri miwili ya
vyombo viwili vya Serikali,
sisi uongozi hatuna ujuzi
wanaoutumia ‘TANSORT’
wa kukadiria kwa muda
malipo ya mrabaha kwa Serikali.
“Yanakamilishwa baada ya
kupatiwa matokeo halisi ya
zabuni ya wazi ya almasi za
WDL na uaminifu wake
unathibitishwa na TANSORT
kutoka wizarani,’’ilieleza
sehemu ya taarifa hiyo.
Kamishna wa Nishati na Madini,
Benjamin Mchwampaka jana
alisema taarifa ya mgodi huo
haijafika kwake bali ameiona
kwenye mitandao ya jamii.
Alisema mpaka sasa hawezi
kujua athari za kusimamisha
uzalishaji wa mgodi huo hadi
atakapopata taarifa rasmi
kutoka kwa uongozi.
“Nimeziona mitandaoni,
sijapata taarifa kutoka
kwao wenyewe itabidi
kuitafakari ikifika kesho (leo).
“Lazima niweze kujua
hilo na niweze kufahamu
pia athari na wamefunga
maeneo gani na athari
hata kwa wafanyakazi
itakuwa kwa kiasi gani ,
’’alisema Mchwampaka.
Hivi karibuni wafanyakazi
wa Uwanja wa Ndege
wa Kimataifa wa Julius
Nyerere (JNIA), walikamata
mzigo wenye madini ya almasi
yenye uzito wa kilo 29, dakika
tano kabla ya ndege kupaa,
huku yakiwa yameandikwa yana kilo 14.3.
Inaelezwa walioshiriki kufanya
udanganyifu huo ni watumishi
wa serikali waliopewa dhamana
ya ukaguzi na uthaminishaji
katika mchakato wa kuanzia
mgodini hadi kuidhinisha
usafirishaji wa madini hayo nje ya nchi.
Waziri wa Fedha na Mipango,
Dk.Philip Mpango, juzi alitembelea
uwanja wa JNIA kwa ajili ya kutoa
maagizo kwa Mkurugenzi Mkuu wa
Mashitaka (DPP), Mganga Biswalo.
Alisema Tanzania imepigwa vya
kutosha hivyo wote waliohusika
katika udanganyifu huo washughulikiwe
kwa mujibu wa sheria.
Waziri alisema wafanyakazi wote
waliohusika kuanzia hatua ya
uchimbaji wa madini hayo
mpaka kule yanakosafirishwa,
wamulikwe na vyombo
vya dola kubaini uhalali wa
mali zao wanazomiliki.
Ilielezwa kuwa wamiliki wa
mgodi wa madini hayo walisema
yana thamani ya Dola za
Marekani milioni 14.8, lakini
baada ya uchunguzi ilibainika
thamani yake ni Dola za
Marekani milioni 29.7.
No comments